Jumamosi, 4 Juni 2016

RIWAYA YA DAIMA SEHEMU YA 2



RIWAYA: Daima
NA: Frank Masai
MAWASILIANO: 0717 738973
SEHEMU YA 2

ILIPOISHIA.


Wakati Fatma anaendelea kuzagaa pale uwani akiitazama nyumba ile juu ya bati na anga zima la pale alipohamia, alijikuta akigongana na mtu ambaye hakumjua hapo kabla.
 Alikuwa ni mtoto usawa wake, lakini yeye ni wa kiume na alikuwa kabeba baadhi ya vitu vidogovidogo vya kupeleka ndani ya nyumba ile.
Akamtazama yule mvulana kwa macho yake machanga, na mvulana yule akamtazama pia. Macho yao yakagongana. Wote kwa pamoja wakabaki hawana la kusema.

“Sam peleka vitu ndani,” Ni sauti ya mtoto mwingine ilimsihi mtoto mwenzake apeleke vitu ambavyo kavikamata mikononi mwake.
Alikuwa Samson, kijana anayelelewa katika mazingira magumu akiwa na mama yake. Samson akatabasamu mbele ya Fatma, na Fatma akajibu tabasamu lile kwa kukenua hadi mapengo yake ya mbele yakaonekana. Samson akaingiza vitu vile ndani.

ENJOY.

Macho ya Fatma, hayakuacha kumfatilia Samson ambaye baada ya kuingia ndani, naye binti aliingia ndani huku kichwani mwake akili za kitoto zikiwa zimeenea kana kwamba alikuwa anataka kujua zaidi kuhusu mtoto mwenzake.

Akaingia ndani na kumkuta Sam akiwa anaweka kwa uangalifu vitu ambavyo alikuwa ameagizwa avipeleke ndani.

“Unaitwa nani?” Fatma alimuuliza Sam na mtoto yule aligeuka nyuma kwa kasi na kukutana na cheko ya kitoto toka kwa Fatma. “Nimekushtua eeh.” Alitania na Sam akawa hana budi naye kutabasamu.

“Naitwa Samson,” Akajibu Sam kwa sauti ya kitoto.

“Samson au Sam?” Akauliza mtoto yule mwenye asili ya Kiarabu na weusi wa Kiafrika.

“Sam wanalikatisha tu! Ila naitwa Samson.”

“Haya Samson. Mi’ naitwa Fatma.” Akajitambulisha mtoto wa kike.

“Ahaaa! Fatma. Unafanana na mama.” Akaongea Sam huku bado naye uso wake umepambwa na tabasamu.

“Ndio. Na ndio maana anani…” Mara walikatishwa maongezi yao.

“Wewe Sam, kachukue vitu vingine nje. Unamjua huyo, utanyongwa.” Mtoto mwenzake aliongea na kumfanya Samson atoke haraka mle ndani na kuendelea na kazi ambayo ameitiwa huku Fatma kila mara akiwa anamuangalia na kutabasamu kana kwamba alikuwa anamfahamu Samson kwa muda mrefu..
****
“Baba, yule pale nataka awe rafiki yangu.” Baada ya kazi kumalizika, Fatma alimfuata baba yake na kumwambia maneno hayo.
Kwa muda huo Sam na watoto wenzake walikuwa wanafuraha baada ya kupewa ujira wao ambao japo haukuwa mkubwa, lakini kwao waliona kama neema imewadondokea.

“Hapana mwanangu. Kuna marafiki utawapata, lakini si hawa wa huku. Kwanza wachafu. Embu angalia, wewe unaweza kucheza na mtoto kama yule?” Baba yake Fatma, Bwana Abdul, aliongea kwa dharau na kumfadhahisha mwanaye.

“Baba mimi sitaki bwana, nataka yule.” Fatma akadeka na kumkasirisha baba yake.

“….Embu niondokee hapa.” Abdul alimfukuza mwanaye baada ya maneno makali aliyompatia kuhusu Sam. Mtoto yule hakuwa na pa kukimbilia zaidi ya kwa mama yake ambaye naye alikuwa roho juu baada ya kumuona mtoto wake wa pekee akifokewa kana kwamba alikuwa kafanya kosa kubwa.

“Nyamaza. Usilie mwanangu eeh! Nyamaza, nitamchapa baba yako.” Alimbembeleza mwanaye, Johari Bin Said Mustapha. Kisha akamgeukia mumewe, “Usipende kumkera mtoto, nakuomba Abdul.” Johari alijikuta akibwatuka kwa ukali bila hata kuzirekebisha hisia zake za maumivu. Abdul akajikuta mwenye kugwaya hasa alipogundua kuwa Fatma ndio jicho na pia moyo wa mkewe. Ni kheri umchukue yeye Johari, ukamchuna ngozi, ukampaka ndimu na pilipili na kisha ukambanika, halafu baadaye ukawatupia mbwa wafanye kitoweo kuliko kumsinya kidogo Fatma hata kama amekosea.

“Johari mke wangu, unamdekeza huyu mtoto, baadae itakuja kutu-cost.” Aliongea kwa upole Abdul, mume wa Johari.

“Simdekezi. Namlea kwa upendo. Tumuache mtoto naye ajichanganye na watoto wenzake anaowachagua. This is just a world, you will never know who is going to burry you.” Johari aliongea kwa hisia akimuelekeza mumewe kuwa hii ni dunia tu, huwezi kujua ni nani atakayekuja kukuzika.

Ipo hivi, Bwana Abdul ni mtu ambaye haamini kama masikini wanaweza kumsaidia yeye katika maisha yake. Na imani hiyo ilikuwa inapingwa vikali sana na mkewe Johari. Hiyo ndio sababu mara nyingi sana watu hawa hukwazana hasa linapokuja suala la ushirikiano baina ya masikini na matajiri. 

“Siku moja utaniamini nachokwambia.”Aliongea Abdul na kuingia ndani akimuacha mkewe anamuangalia kwa macho yaliyojaa ugwadu wa hasira pamoja na kisununu.

“Twende ndani mwanangu.” Huo ndio uamuzi aliouchukua yule mwanadada ambaye alionekana hapendi sana matendo ya mumewe, hasa ya kibaguzi.
****
“Mamaa… Mamaa… Mamaa…” Samson, alikuwa anamuita mama yake huku kasi ya miguu yake ikiwa kubwa kukimbia kule ambapo nyumba anayoishi na mzazi wake ipo.

“Nini tena mwanangu?” Aliuliza Mama Samson kwa kihoro akidhani labda mwanaye anafukuzwa na mtu au labda kuna janga limemkuta.

“Nimekuletea hela mama.” Aliongea Samson baada ya kufika mbele ya mama yake. Mama wa Samson, akafuta machozi ambayo yalikuwa yanamuandama kwa sababu ya kupikia kuni ndani ya chumba kidogo mithili ya choo. Alikuwa kavaa mavazi ambayo hayana hadhi kubwa lakini aliamini kuwa yeye si kama hao wanaojiita wenye hadhi.

“Nani kakupa mwanangu?” Aliulizwa Samson na mama yake.

“Pale kwenye lile jumba kubwa wanahamia. Tumewasaidia nd’o wakanipa hiyo.” Aliongea Samson kwa furaha huku akizidi kuusogeza mkono wake ili mama yake aichukue ile fedha.
Mama Samson akatabasamu kwa furaha na badala ya kupokea ile hela, alipapasa kichwa cha mwanaye huku akijaribu kutafakari la kumwambia.

“Hiyo ni yako Sam. Kaitumie unavyotaka. Jukumu lako ni kujitafutia kwa sasa. Lakini jukumu langu mimi ni kukutafutia. Ipo siku na wewe utakuwa na jukumu hilo, kwa sasa bado hujafikia umri huo. Kwa hiyo utakachokipata, jua kuwa umejitafutia na sina haki ya kukitumia.” Aliongea mama yake ambaye alikuwa ni mwema na mwenye sauti ya hekima na utii hata kwa watoto wadogo.

“Lakini mama, wewe unahitaji hela hii kuliko mimi ninavyoihitaji. Sina mamlaka na hii fedha kama ulivyokuwa nayo wewe. Kwa nini usiichukue uifanyie kazi ambayo itatusaidia sote hapa nyumbani?” Wanasema mtoto wa nyoka ni nyoka. Ni wazi hata Samson alikuwa na ulimi sawa na ule wa mama yake.

“Unajua nini mwanangu?” Mama Samson, alichutama na kukishika kichwa cha mwanaye kwa mikono miwili. “Kuna muda unatakiwa kuitambua thamani ya mzazi. Na kuna muda unatakiwa kujua unathaminiwa na mzazi. Kwa sasa unatakiwa kutambua kuwa unathaminiwa na si wewe kuthamini japo ni vema unithamini, lakini si kwa njia hii,” Aliongea bado kwa utulivu yule mama. “Umewasaidia wazazi wengine, na wao kwa hekima zao, wamekulipa. Lakini haimaanishi kuwa wamekupa ili uje utumie na mimi bali ukajifariji wewe kwa kazi uliyoifanya.”

“Ndio. Lakini mimi nimekupa wewe kwa sababu sina matumizi nayo. Nitaenda kuchezea tu huko kwa kula pipi na jojo, lakini wewe unaweza kununulia mkaa na ukapika kwa uhuru kuliko sasa hivi.” Mama Samson akatabasamu na kutikisa kichwa kwa maneno ya mwanaye. Akashindwa la kuongea na badala yake akasimama na kumuangalia tena mwanaye, safari hii kwa upendo zaidi.

“Haya.Nipe, maana umenishinda kwa kutoa hamasa.” Sam akafurahi baada ya ushawishi kwa kupenya kwenye ukuta mzito wa akili ya mama yake. Akampa kiasi cha shilingi elfu mbili mama yake na kisha akamkumbatia kabla hajamuachia na kurudi kwa wenzake kuendelea kucheza. Mama wa mtoto akawa anamuangalia asiamini kama kapata utatijiri wa njia nyingine kabisa, utajiri wa mtoto mwenye hekima.
****
Miaka miwili ikaingia. Hali ya umasikini ikawa bado imetawala kwa Edna, mzazi wa Sam. Aliishi kwa kubangaiza na kiasi alichokipata, alikuwa anakiweka kwa ajili ya mwanaye kwenda shule. Na hatimaye, Sam akaanza shule ya msingi akiwa na miaka tisa.

Wakati yeye anaanza shule katika umri ule, tayari Fatma alikwishaanza shule punde tu alipohamia katika ule mtaa. Urafiki wa hawa watoto ulikuwepo lakini ulikuwa unapingwa vikali sana na baba mtu. Mara kadhaa Mama Samson, Bi Edna, alipelekewa onyo na yule bwana kana kwamba mama alikuwa anahusika na urafiki wa watoto. Mama Sam alikuwa mwenye ulimi wa staha, na wenye kumuelewesha kila aliyekuwa na sikio. Lakini Bwana Abdul, alikuwa haoni wala sikio lake halikufunguka licha ya kutiwa ufunguo wa kufunguliwa.

“Mama samahani, samahani sana mama yangu.” Ni sauti ya Johari kila tukio likitokea ndio ilikuwa inaomba msamaha. Mama wa watu alikuwa mwenye kutabasamu na kuacha mambo yale yapite. Johari alikuwa anajaribu kumpa pesa yule mama lakini kwa bahati mbaya, hakuna hela ambayo Mama Samson aliweza kuikubali. Aliamini msamaha wa kweli unatoka moyoni na si kwa kutumia pochi zinazokaa kwapani au kwa wanaume kukaa nyuma ya kalio.

“Pesa si kitu mwanangu. Kaa na mumeo, mwambie dunia inalizunguka jua na pia inajizungusha yenyewe bila kuchoka. Hapa na maana kwamba, ipo siku atajua thamani ya mtu ni bora kuliko vitu. Sitachoka kuisubiri siku hiyo, mimi ni dunia.” Maneno hayo yalikuwa yanajirudia mara kwa mara kichwani mwa Johari. Alishindwa kumwambia mumewe kwa sababu alijua hatotilia maanani lolote lile.

Watoto wawili wakiwa katika furaha juu ya urafiki wao, huku upande mmoja wa wazazi ukiwa hautaki hata kusikia habari hizo, wanaamua kufanya jambo. Jambo ambalo liliweza kuwaweka pamoja kwa muda mrefu sana.

“Sam.” Siku moja binti mwenye umri wa miaka saba, Fatma. Alimuita rafiki yake kwa kificho getini kwao. Sam akimbilia pale getini na kumsikiliza. “Unajua baba hapendi urafiki wetu. Sasa tunafanyaje?” Binti akataka suluhu ya urafiki wao.

“Sijui la kufanya Fatma. Ila nachojua, MUNGU ni mwema kwetu sote. Hajatuumba ili tusijuane, bali katuumba ili tujuane na ndio maana tupo hapa leo. Licha ya mimi kukujua wewe na wewe kunijua mimi, pia kanijulisha mimi Wazazi wako wapo vipi na kakujulisha wewe na wazazi wako juu ya mzazi wangu. Nachoamini kwa sasa, urafiki wetu utakuwa ni wetu. Hakuna ambaye anatakiwa kuja kati yetu.” Samson aliongea maneno ya kujiamini bila kujua athali za maneno yake.

“Nimefuahi kusikia hayo Sam. Rafiki ndiye kiongozi sahihi wa kichwa cha yeyote kwa sababu rafiki ndiye anakuja kukufuta chozi pale familia yako inapokutoka. Na rafiki ndiye awezaye kukuliwaza pale unapokwazana na wazazi wako. Hamna mtu wa muhimu kama rafiki. Kama huna rafiki, basi dunia hii utaiona inaegemea upande mmoja hasa pale unapokwama mahali.” Aliongeza maneno hayo Fatma na kumfanya Sam atabasamu. “Niahidi utakuwa rafiki yangu DAIMA.” Akaongeza Fatma huku anatoa kidole chake kidogo kwenye tobo la geti. Samson akakipokea kidole kile kwa kuunga na kidole chake.

“Nakuahidi utakuwa rafiki yangu DAIMA.” Akajiapisha rasmi Samson.

“DAIMA.” Akaongea maneno hayo Fatma kama msisitizo.

“Ni DAIMA.” Naye Sam akasisitiza.

ITAENDELEA.

Maoni 1 :
Write maoni