Ijumaa, 10 Juni 2016

Rais Magufuli awaapisha Jaji Lila na Jaji Wambali na aagana na Balozi wa Oman nchini

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 10 Juni, 2016 amemuapisha Mhe. Jaji Shaaban Ali Lila kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Ikulu Jijini Dar es salaam.
Kabla ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Jaji Shaaban Ali Lila alikuwa Jaji Kiongozi.
Wakati huohuo, Rais Magufuli amemuapisha Mhe. Jaji Ferdinand Leons Katipwa Wambali kuwa Jaji Kiongozi. Kabla ya kuteuliwa na kuapishwa kuwa Jaji Kiongozi, Mhe. Jaji Ferdinand Leons Katipwa Wambali alikuwa Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mkoani Tanga.
Jaji Kiongozi Mhe. Ferdinand Leons Katipwa Wambali amechukua nafasi iliyoachwa wazi na Mhe. Jaji Shaaban Ali Lila ambaye amekua Jaji wa Mahakama ya Rufani.




 Katika hatua nyingine, Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameagana na Balozi wa Oman hapa nchini Mhe. Saoud Ali Mohamed al Ruqaishi ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.
Akizungumza na Balozi huyo, Ikulu Jijini Dar es salaam Rais Magufuli ameishukuru Oman kwa kuendeleza ushirikiano na uhusiano wa kihistoria na kidugu na Tanzania, na ameahidi kuwa serikali yake ya awamu ya tano ipo tayari kuongeza ushirikiano huo.
Mhe. Rais Magufuli pia amemuomba Balozi Saoud Ali Mohamed al Ruqaishi kufikisha salamu zake kwa Sultani wa Oman Mtukufu Qaboos bin Said al Said na kumueleza kuwa Tanzania inawakaribisha wawekezaji na wafanyabiashara wa Oman na inatarajia kuona miradi ya ushirikiano katika uwekezaji ukiwemo mradi wa Bagamoyo inaanza kutekelezwa haraka.
“Naomba umfikishie salamu zangu za dhati Mtukufu Qaboos bin Said al Said, Sultan wa Oman na umwambie tunamkaribisha Tanzania na nitafurahi kuona mradi wa uwekezaji wa Bagamoyo unakuwa kielezo cha undugu na urafiki wetu uliodumu kwa miaka mingi” Amesema Rais Magufuli.
Tanzania kwa kushirikiana na nchi za Oman na China zimekubaliana kutekeleza mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo Mkoani Pwani.



Hakuna maoni:
Write maoni