Alhamisi, 2 Juni 2016

RIWAYA MPYA




RIWAYA: Daima
NA: Frank Masai
MAWASILIANO: 0717 738973
SEHEMU YA 1

Hisia za mapenzi hujengwa pale mioyo ya wawili inapokuja pamoja na kujigundua kuwa inaendana. Hisia za mapenzi ndizo hujenga mapenzi na kuyafanya yaishi katika mioyo ya wawili waliokutana katika dunia hii ambayo watu huuita kila jina zuri na baya.

Mapenzi ni njia ambayo kila moyo hupenda kuipita hata bila kutaka. Na katika kila moyo ambao unajiingiza katika mapenzi, basi kuna moyo unapitia magumu ambayo huweza kutiririsha machozi wakati magumu hayo yanapita.

Wanasema penzi la kweli si rahisi kufa. Usemi huu ni kweli na hamna cha kukataa katika hili. Pale mioyo miwili inapokuja na kuungana, basi hutengeza kitu ka bomu la nyukilia, linapolipuka basi huwa maafa na uharibifu mkubwa.

Wapo wanaodhani mapenzi ya wawili ni lazima yanedane na dini, kabila, elimu au kipato. Na wapo wanaodhani kuwa mapenzi hayaendani na hivi vitu. Wengi wataungana na kauli ya mwisho, labda kwa sababu hawajui sera za familia fulani. Mimi ni mmoja wao nisiyeamini kuwa mapenzi yanajengwa kwa njia za kuangalia dini, kabila au kipato na elimu.

Kama na wewe unaamini hili, ni vipi unaweza kupigana kuliokoa penzi lililomea katika mioyo yenu? Kama mmoja ambaye siamini kuhusu udini, kabila, ukipato na elimu, naweza kumshauri yule aliyetokewa na jambo hili, apigane kufa na kupona ili kuliweka penzi lake hai.
****

Sauti ya faraja katika masikio ya mama mmoja ambaye alikuwa hoi taabani katika hospitali moja ya nchi ya Tanzania, ilipenya katika ngoma zake na hapo hapo alishusha pumzi ndefu ya imani na kujilaza kifudi fudi katika kitanda cha hospitali ile.
Alikuwa amekaa katika hospitali ile kwa jumla ya siku tano bila kufanikiwa katika kile ambacho kilimpeleka pale.

Alikuwa kafikisha siku za kuweza kujifungua na ndipo alipokimbizwa hospitali ile kwa msaada wa wasamaria wema ambao siku zote walilipa fadhila ambazo mama yule alikuwa anazitenda kwao. Hata wauguzi walipomuona mama yule ndiye kaletwa kwa ajili ya kujifungua, walikuwa wenye kila hali ya utu katika kumpa huduma mama yule ambaye licha ya kutokuwa na kitu katika maisha yake, hasa hivi vya kuonekana lakini moyo na kichwa chake vilijaa ubinadamu wa kutosha. Alikuwa na ulimi wa kuweza kumfanya nyoka asiweze kumng’ata liyemdhamiria. Alikuwa na kinywa safi ambacho ndicho kilimfanya aheshimike na kila mtu, kila rika na kila jinsia.

Sauti ya mtoto mchanga, ilisikika ikilia kwa nguvu baada ya kutoka tumboni kwa mama yake. Wauguzi waliyobeba jukumu la kumleta mwana yule duniani, walitabasamu na kumtazama mama aliyehusika kumlea mwana yule kwa miezi tisa akiwa tumboni. Wakatabasamu zaidi pale mama yule alipowauliza kwa sauti ya kichovu kuhusu jinsia ya mwana yule.

“Ni wa kiume.” Alijibu muuguzi mmoja wa kike aliyekuwa kamkamata mtoto na mama yule alitabasamu pamoja na wauguzi, kisha kwa sababu ya kutumia nguvu nyingi kwa kumleta duniani mwana yule, alifumba macho yake, mama yule alipoteza fahamu..
****
Jogoo aliwika katika nyumba moja kuu-kuu iliyokuwa imeezekwa kwa nyasi juu yake, na kujengwa kwa tope bila tofali. Jogoo kuwika ilikuwa ni ishara ya mapambazuko, ilikuwa ni sauti ya kuwakumbusha watu waamke na kwenda eidha kulijenga taifa au kulisafisha taifa. Ni siku mpya ilikuwa inaanza, siku ambayo nyumba hii ilipata mgeni mpya, mgeni ambaye aliletwa na mama pendwa katika sehemu ile anayoishi.

Aliyekabidhiwa kuitazama nyumba ile kwa wema, alidamka baada ya jogoo kuwika mara kadhaa, na kitendo bila kuchelewa alianza kazi ya usafi wa mazingira ya nje ya nyumba ile. Alionekana wazi alikuwa na hamasa ya jambo fulani kwani hata wakati fagio linatambaa katika ardhi ile kuondoa uchafu, yeye hakuwepo katika dunia hii na badala yake alikuwa anafagia huku ametabasamu kana kwamba hukujali vumbi zito lililokuwa linapenya katika kinywa na pua zake. Alikuwa na furaha mwanamama yule.

Ni wiki mbili zilitimia tangu mama yule wa hospitali apate mtoto wa kiume. Alipata huduma za kutosha toka katika hospitali ile. Wauguzi walitamani mama yule asiondoke katika hospitali ile, lakini walikuwa hawana jinsi kwani muda uliwadia wa mama yule kuanza majukumu mapya ya kumlea mwana wake wa pekee.

Saa nne ya asubuhi, mama aliyekuwa anafagia nje ya nyumba iliyokuwa inaonekana inaukwasi, alifika katika hospitali aliyokuwa kalazwa mama mwenye kiumbe mpya na kumchukua rafiki yake kipenzi tayari kwa kurudi naye nyumbani. Wauguzi waliwapungia mikono ya kheri wakati wazazi wale wanaingia ndani ya usafiri utakao wafikisha nyumbani kwao. Nao wakinamama wale, walijibu kwa kuwapungia mikono pia. Safari ya kwenda kwao ikashika hatamu.
****
Ni furaha kubwa ndio ilikuwa imetawala katika nyumba ya mama aliyekuwa kajifungua. Wakina mama wenzake walipiga vigeregere kila mara walipopata jambo la kujenga. Waume walikuwa wanamiminika na kumpongeza mama yule kwa kumpa chochote cha kheri. Kheri hiyo ndio ilifanya vigeregere kutokwama katika ndimi za wakina mama wale.

“Mwana wetu anaitwa nani huyu,” Baba mmoja wa makamo alimuuliza mama wa mtoto pale alipoenda kumtembelea.

“Anaitwa Samson.” Mama yule alimjibu mzee yule huku tabasamu pana likichomoza katika midomo yake pevu.



“Oooh! Samson!” Mzee yule aliongea huku akisogeza uso wake kwa yule mtoto. “Ni jina la shujaa wa MUNGU. Yule bwana jabari aliyeweza kupambana na simba, kisha akamteketeza bila huruma. Hakutumia silaha katika mpambano wake, ni mikono pekee,” Mzee yule aliongea zaidi huku safari hii akikunja ngumi kuonesha ukakamavu wa kitu ambacho alikuwa anakihadithia. Akaendelea,
“Nadhani MUNGU kamleta shujaa huyu kupambana katika maisha haya. MUNGU kamtuma mwana huyu kwa ajili ya jambo la kishujaa. Naamini atalitimiza. Samson karudi tena.” Maneno hayo yakaamsha vigeregere tena na mama yule alichemka mwili kwa dezo baada ya sifa kede zilizomwagwa na mzee yule.

“Ahsante Mzee Shahibu.” Mama yule alimshukuru mzee yule kwa maneno yake.

“Hapana. Siruhusiwi kushukuriwa, bali kukushukuru wewe kutuletea shujaa. Asante Mama Samson.” Mzee yule aliongea huku akipiga goti na kushika miguu ya Mama Samson.
Hoihoi zikaibuka tena na mama yule alishindwa kustahimili hali ile, akajikuta akitoa machozi, machozi ya furaha.

Chozi ni ishara ya hisia zinazotokana na jambo fulani. Chozi litokapo humaanisha kuguswa na jambo fulani ambalo ni hisia pekee ndizo hutambua siri hiyo. Hakuna chozi liwezalo kudondoka bila kuhusisha hisia. Achana na chozi litokalo labda kwa sababu ya kulala au kuumwa mafua, hapa nazungumzia chozi la hisia ya jambo fulani.
Mama Samson alitoa chozi la hisia za furaha iliyogubikwa katika moyo wake. Hana pesa, hana maisha bora kama wengine, hana kitu chochote cha kumfanya naye azungumzwe mtaani kama tajiri au mtu fulani maarufu. Lakini rafiki zake na majirani, walimuonesha upendo wa dhati licha ya hali yake.
******
BAADA YA MIAKA SABA.

Kikundi kidogo cha watoto kilionekana kikicheza mpira wa manailoni eneo moja lililokuwa lina uwazi mpana wa uwanja. Watoto walifurahia mchezo ule na walitamani usiishe hata kidogo kwani ni starehe moja iliyokuwa inaviweka vichwa vyao sawa.

Wakati mchezo ukizidi kunoga baina ya watoto wale, gari moja kubwa linajongea katika nyumba moja kubwa ambayo ilikuwa imejengwa mitaa ile. Ilikuwa ni nyumba kubwa kupita nyumba zote zilizopo pale mtaani. Ilizunguishiwa uzio mpana wa matofari na nyaya za umeme ziliwaka kila nukta moja ya sekunde ya saa.

Gari ile pana ilisimama nje ya geti na kwa dakika tatu hakushuka mtu hadi pale gari lingine la kifahari lilipojongea na kusimama nyuma ya gari lile kubwa.
Dereva wa gari kubwa alishuka na kwenda kufungua geti lakini kwa bahati mbaya, gari lile pana na refu kwenda juu, likashindwa kuingia ndani na jukumu kubwa lilikuwa ni kutafuta vijana ambao wangeweza kufanya kazi ya kupakuwa na kuingiza ndani baadhi ya vifaa vidogo vidogo.

Watoto waliacha kucheza mpira na kuanza kuangalia uzuri wa gari lililofuatana na lile la mizigo. Wakawa wanalitamani na wengine walilipapasa kwa mshangao mkubwa.

“Watoto, mnaweza kutusaidia kupeleka vitu ndani?” Aliwauliza dereva wa gari kubwa na watoto wote walijibu kwa haraka kuwa wanaweza.
Wakatafutwa na vijana wengine wakubwa na kuanza kushusha mizigo iliyomo kwenye gari. Gari la kifahari liliingizwa ndani na kuwekwa sehemu yake wakati huo watoto walipishana mara kwa mara mlangoni wakiwa wamebeba vitu vya kuingiza ndani.

Katika gari lile la kifahari, mlango wa dereva unafunguliwa na bwana mmoja mrefu na mweusi kiasi akatoka nje akiwa katika mavazi ya gharama labda kushinda ya yeyote katika mtaa ule. Kiatu kirefu cha ngozi ya chatu kinadondokea ardhi na bwana yule anatabasamu baada ya kuangaza huku na huko kwenye ile nyumba.

Upande wa pili baada wa dereva, mlango pia unafunguliwa na anashuka mwanadada mrembo kupindukia, naye akiwa katika mavazi ya gharama kama aliyeshuka upande wa dereva. Huyu alikuwa na asili ya kiarabu kutokana na nywele zake ndefu pamoja na weupe wa asili ambao MUNGU kamuumba nao.

“Abdul, umefanya vema sana mume wangu.” Mwanamke yule aliongea huku kapambwa na tabasamu pana ambalo siku zote alikuwa akilichanua, mumewe kipenzi, Bwana Abdul Abdulah, mmiliki wa makampuni makubwa ya biashara nchini Tanzania, alikuwa hachomoki wala kufikiria kwenda nje ya ndoa yake.

“Tumefanya wote haya mke wangu Johari,” Naye mumewe alijibu huku akibusu midomo mipana ya mkewe ambaye naye si haba, alikuwa anafukuzana na mumewe katika ujasiriamali.
Wakati hayo yanaendelea, mlango wa abiria wa gari lao nao unafunguka na mtoto wa miaka ipatayo sita anashuka ndani ya gari lile. Alikuwa ni mtoto wa kike ambaye alichukua sura nzuri ya mwanamke anayepongezana na Abdul, namzungumzia Johari Said Mustapha.

“Baba hapa ndio kwetu kupya?” Mtoto yule alimuuliza baba yake, Bwana Abdul.

“Ndio Fatma. Utakaa hapa na dada zako wa kule,” Aliongea Abdul huku akijaribu kumwambia kuwa atakaa na wafanyakazi aliotoka nao huko.
Mtoto yule akatabasamu na kuanza kuangaza huku na huko ndani ya mjengo ule ambao kwa hakika ulijengwa kwa ustadi na ramani za kileo zaidi.

Wakati Fatma anaendelea kuzagaa pale uwani akiitazama nyumba ile juu ya bati na anga zima la pale alipohamia, alijikuta akigongana na mtu ambaye hakumjua hapo kabla.
 Alikuwa ni mtoto usawa wake, lakini yeye ni wa kiume na alikuwa kabeba baadhi ya vitu vidogovidogo vya kupeleka ndani ya nyumba ile.
Akamtazama yule mvulana kwa macho yake machanga, na mvulana yule akamtazama pia. Macho yao yakagongana. Wote kwa pamoja wakabaki hawana la kusema.

“Sam peleka vitu ndani,” Ni sauti ya mtoto mwingine ilimsihi mtoto mwenzake apeleke vitu ambavyo kavikamata mikononi mwake.
Alikuwa Samson, kijana anayelelewa katika mazingira magumu akiwa na mama yake. Samson akatabasamu mbele ya Fatma, na Fatma akajibu tabasamu lile kwa kukenua hadi mapengo yake ya mbele yakaonekana. Samson akaingiza vitu vile ndani.

ITAENDELEA.

Hakuna maoni:
Write maoni